Waziri wa mambo ya nje wa Kenya Dkt. Alfred Mutua amepinga madai ya Umoja wa Mataifa kuwa mamlaka za serikali zinatumia nguvu kupita kiasi kuzima maandamano ya kuipinga serikali kote nchini.
Haya yanajiri baada ya msemaji wa Ofisi ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa, Jeremy Laurence, kusema kuwa shirika hilo "limesikitishwa sana na ghasia zilizoenea, na madai ya matumizi ya nguvu yasiyo ya lazima , ikiwa ni pamoja na matumizi ya silaha za moto, na polisi wakati wa maandamano yanayoongozwa na Muungano wa Azimio la Umoja."
Akizungumza leo Bw Mutua aliitaja kauli hiyo ya Umoja wa Mataifa kama propaganda zisizo sahihi na za kupotosha zinazolenga kuwanyima Wakenya uhuru wao wa kidemokrasia.