Waziri Mkuu wa Iraq, Mustafa al-Kadhimi amenusurika katika jaribio la mauaji lililohusisha ndege inayorushwa bila rubani (Drone) iliyolenga makazi yake huko Baghdad, ambapo walinzi wake sita wamejeruhiwa.
Waziri mkuu huyo alijitokeza na kusema kuwa hajaumizwa na jaribio hilo na anaendelea vizuri. "Asante Mungu, niko sawa na niko miongoni mwa watu wangu,” alitweet kwenye akaunti yake ya Twitter.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Saad Maan aliiambia televisheni ya taifa ya al-Iraqiya kuwa vikosi vya usalama vilidungua ndege mbili huku ya tatu ikifanikiwa kugonga makaazi ya al-Kadhimi.
“Al-Kadhimi hakudhurika, ila baadhi ya watu ndani ya nyumba wamepata majeraha. Wanapokea matibabu, "Maan amesema huku akikataa kutoa maelezo mengine. Mpaka sasa hakuna kundi lolote linalohusishwa na shambulizi hilo.