WAZIRI wa Afya, Mutahi Kagwe na Gavana wa Kakamega, Wycliffe Oparanya, wameonja joto ya jiwe baada ya msafara wao kurushiwa mawe na wananchi waliokuwa na hasira kutokana na ukosefu wa vifaa vya kujikinga na maambukizi ya virusi vya corona.
Wananchi hao walizuia msafara wa viongozi hao katika eneo la Kakamega, wakitaka kufikisha malalamiko yao kuhusu kukosekana kwa barakoa na vitakasa mikono katika kaunti hiyo, hali inayowafanya kuwa katika hatari ya kuambukizwa virusi vya corona vinavyosababisha ugonjwa hatari wa Covid-19.
Viongozi hao walikumbana na tukio hilo baada ya kuingia katika mji huo, ambapo walilazimika kuomba msaada kutoka Jeshi la Polisi. Polisi walifika katika eneo hilo na kutumia nguvu kutawanya umati uliokuwa ukiwarushia mawe msafara wa viongozi hao.
Wananchi hao walimlalamikia Kagwe kuwa mikakati ya kukabiliana na maambukizi ya corona, inawabagua kwa kutowapatia vifaa vya kujikinga na virusi hivyo hatari vilivyotikisa dunia.
“Hatukutaki hapa, nenda Nairobi, huku hakuna corona. Barakoa zote umepeleka Nairobi, hatuna vitakasa mikono, hatuwataki, tunataka vitakasa mikono pamoja na barakoa,” alisema mmoja wa wananchi hao.