Ankara.Polisi katika mji mkuu wa Uturuki, Ankara wamewakamata watu watano wanaotuhumiwa kuwa wapiganaji wa kundi linalojiita Dola la Kiislamu (IS) kwa madai ya kupanga mashambulizi katika mkesha wa mwaka mpya.
Shirika la habari la Uturuki, Anadolu, limeripoti kuwa watuhumiwa hao ni raia wa kigeni wanaofungamana na makundi ya kigaidi nchini Syria na Iraq.
Anadolu imesema msako wa polisi unaendelea na huenda watu zaidi wakakamatwa.
Taarifa hiyo imetolewa wakati hatua za kiusalama zikiendelea kuchukuliwa nchi nzima kabla ya sherehe za mwaka mpya.
Kwa mujibu wa wizara ya mambo ya ndani ya Uturuki, iliyonukuliwa na Sauti ya Ujerumani (DW) zaidi ya askari 317,000 wa usalama wametawanywa nchini humo.
Kwa mujibu wa Anadolu, zaidi ya watu 100 wanaotuhumiwa kuwa wapiganaji wa IS wakiwamo raia 50 wa kigeni, walikamatwa katika msako unaoendelea nchi nzima.