Mamlaka ya Malawi inasema watu sita wamefariki na wanne kujeruhiwa kutokana na mafuriko ya wiki iliyopita katikati mwa nchi.
Zaidi ya watu 14,000 wamelazimika kuyahama makazi yao, huku wengi wao wakiwa wamekaa kambini, Idara ya Masuala ya Kukabiliana na Majanga nchini humo ilisema katika taarifa yake Jumanne.
Imesema maeneo mengi ambayo yameathiriwa na mafuriko hayo bado hayafikiki kutokana na uharibifu mkubwa wa barabara na miundombinu mingine.
Hali hii imetatiza utoaji wa misaada, ilisema, huku wafanyakazi wa kibinadamu wakitegemea zaidi boti kufikia maeneo yaliyoathirika.
Shirika hilo limeomba msaada zaidi kutoka kwa watu binafsi, makampuni na mashirika ya misaada ili kuunga mkono juhudi za serikali za kutoa misaada.
Tukio hili limetokea ikiwa ni mwaka mmoja tu baada ya mamia ya Wamalawi kupoteza maisha baada ya kimbunga Freddy kupiga kusini mwa Afrika.