SHIRIKA la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu (UNFPA) limesema idadi ya watu nchini wanaohitaji misaada imeongezeka kutoka milioni 7.5 mwaka jana mpaka milioni 8.3. Sudan Kusini inakadiriwa kuwa na watu zaidi ya milioni 11.
Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayoratibu masuala ya kibinadamu (Ocha) nchini Sudan Kusini imesema kuwa, miaka ambayo nchi hiyo imekuwa na migogoro, mabadiliko ya hali ya hewa na sasa mlipuko wa ugonjwa wa covid-19 imesababisha ongezeko la wahitaji kwa watu wengi.
Kati ya wahitaji hao wapo wakimbizi na wanaotafuta hifadhi 310,000. “Migogoro, ukosefu wa usalama na majanga ya asili yamefanya karibu watu milioni nne kukimbia makazi yao kuanzia mwaka 2013,” ilisema ofisi hiyo na kwamba upungufu wa chakula umeongezeka kwa watu zaidi ya milioni 7.2 mwaka huu.
Ofisi hiyo imesema mafuriko yameathiri watu takribani milioni moja kipindi cha mwaka 2019 -2020, huku nchi ikiendelea kuathirika kwa kiasi kikubwa na mlipuko wa virusi vya corona kutokana na kukosekana kwa usambazaji wa vifaa tiba pamoja na mifumo mibaya ya utoaji huduma za afya, huku kukiwa na changamoto ya jamii kutozingatia masuala ya usafi.