Idadi isiyojulikana ya wanakijiji wanahofiwa kukwama baada ya maporomoko ya ardhi kukumba eneo la Kimende, Kaunti ya Kiambu nchini Kenya.
Kisa hicho kilitokea usiku wa kuamkia Jumanne baada ya mvua kubwa iliyonyesha katika eneo hilo, ambayo inaarifiwa kusababisha mafuriko.
Picha zilizoonekana mtandaoni zilionesha nyumba kadhaa zimefunikwa na maporomoko ya matope. Kufuatia tukio hilo, eneo hilo limezingirwa na kutangazwa kuwa eneo hatari, Shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya lilisema.
Ingawa hakuna vifo vilivyothibitishwa hadi sasa, watu kadhaa bado hawajulikani waliko, shirika la misaada liliongeza.
Juhudi za uokoaji zimepangwa kurejea Jumatano. Kuna hofu kuwa maporomoko hayo yanaweza kuvamia maeneo ya jirani huku mvua zikiendelea kunyesha.
Jumla ya watu 289 wamefariki na wengine zaidi ya 280,000 kuhama makazi yao baada ya wiki kadhaa za mvua kubwa kunyesha kote nchini.