Watu wasiopungua 80 wamefariki dunia baada ya boti kuzama mtoni Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC).
Hayo yamebainishwa jana Jumatano Juni 12, 2024 na Rais wa nchi hiyo, Felix Tshisekedi alipokuwa akitoa taarifa kwa vyombo vya habari.
Ajali hiyo ilitokea katika Mto Kwa uliopo kilomita 70 kutoka Mji wa Mushie, Jimbo la Mai-Ndomba karibu na mpaka na Congo-Brazzaville.
Katika taarifa yake kupitia mitandao ya kijamii Rais Tshisekedi amesema: “Amesikitishwa.”
Rais huyo amesema wote walioathirika watapatiwa msaada huku akitaka uchunguzi kufanyika ili kujua kilichosababisha ajali hiyo.
“Rais wa Jamhuri anataka uchunguzi wa kufahamu sababu hasa za tukio hilo, na kuzuia majanga kama hayo kutokea tena siku za usoni,” inasema Ikulu ya DRC kupitia mtandao wa X.
Ajali za boti ni matukio ya kawaida katika nchi ya DRC, vyombo hujaza abiria kupita kiasi, wengi wakiwa hawajui kuogelea na wanasafiri bila maboya ya kuelea.