Watu wasiopungua 27 wameuawa na makumi ya wengine wamejeruhiwa katika mapigano yaliyotokea kwenye maeneo ya magharibi na kusini ya Sudan.
Mashuhuda wamesema, katika matukio tofauti, mapigano yamezuka kwenye eneo tete kiusalama la Darfur yaliyochochewa na ugomvi mkubwa wa kugombea ardhi na kusababisha watu 16 kuuawa.
Watu wengine 11 wameuawa katika jimbo la Kordofan Kusini baada ya ugomvi baina ya watu wawili kupamba moto na kuishia kwenye mapigano ya kufyatuliana risasi.
Machafuko hayo yanaripotiwa huku Sudan ikiwa imegubikwa na wimbi la machafuko yaliyosababishwa na mapinduzi ya kijeshi ya Oktoba mwaka uliopita yaliyoongozwa na mkuu wa jeshi Jenerali Abdel Fattah al-Burhan.
Ripoti zinasema, katika jimbo la Darfur Magharibi linalopakana na Chad, mapigano yalizuka karibu na Kolbus, eneo lililoko umbali wa kilomita 160 kutoka El Geneina, makao makuu ya jimbo hilo, ambapo washambuliaji waliviteketeza kwa moto vijiji vya eneo hilo.