Afisa mmoja wa serikali ya Rwanda amesema kuwa, watu 16 wamethibitishwa kupoteza maisha baada ya mashua kupinduka kwenye mto wa mashariki mwa Rwanda.
Meya wa Wilaya ya Rwamagana, Radjab Mbonyumuvunyi alithibitisha taarifa hiyo jana na kuongeza kuwa ajali hiyo ilitokea Ijumaa jioni kwenye Mto Mugesera wa wilaya hiyio.
Boti hiyo ilikuwa imebeba abiria, hasa wakulima waliokuwa wakitoka kuvuna mazao yao katika tarafa ya Rukumberi wilayani Ngoma, na walikuwa wanaelekea wilayani Rwamagana, wakati upepo mkali ulipovuma na kupelekea boti hiyo kupindukia na baadaye kuzama kabisa.
Katika sehemu moja ya taarifa yake hiyo ya jana, Radjab Mbonyumuvunyi amesema: "Kufikia Jumamosi jioni, miili 14 ilikuwa imeshapatikana na wengine wawili ambao walikuwa bado hawajulikani waliko walipatikana Jumapili."
Pia amesema: "Watu 47 walikuwemo kwenye mashua hiyo wakati ilipozama na si 46 kama ilivyoripotiwa awali. Maafisa wa uwokozi wa majini wamefanikiwa kuokoa watu 31"
Mbonyumuvunyi pia amesema, boti hiyo ilikuwa imejaza kupita kiasi, abiria na mazao ya kilimo yakiwamo mahindi na maharage.