Takriban watu watano walilazwa hospitalini wakiwa na majeraha baada ya kupigwa risasi wakati wa makabiliano kati ya polisi na mshukiwa anayesakwa.
Waathiriwa waliolazwa katika Hospitali ya Kitaifa Kenyatta walipata majeraha mengi baada ya nyumba zao kunyeshewa risasi wakati Mshukiwa wa wizi aliyekuwa akisakwa alipigwa risasi na kuuawa katika majibizano ya risasi katika eneo la Githurai, Nairobi.
Polisi walisema Samuel Karui almaarufu Sammy Steppa alisakwa kwa msururu wa wizi, vurugu na matukio ya mauaji katika eneo la Kasarani na mazingira yake.
Alikabiliwa na polisi katika nyumba ambayo ilisemekana kuwa ya mpenzi wakati alipokuwa amemtebela na rafikiye ambaye alitajwa kuhusika naye kutekeleza hualifu.
Polisi walisema kuwa mshirika wake alifanikiwa kutoroka ingawa walipata bastola,Mkuu wa polisi wa Nairobi Adamson Bungei alisema wanachunguza tukio hilo.
“Tutafuatilia suala hilo,Waliojeruhiwa hali zao zinaendelea vizuri hospitalini," alisema.
Mpenzi wa mshukiwa huyo alikamatwa na kuwekwa chini ya ulinzi wa polisi kwa uchunguzi zaidi.
Mwezi uliopita, afisa wa polisi alipigwa risasi na kuuawa huku wengine watatu wakijeruhiwa katika makabiliano sawa na hayo katika eneo hilo hilo.