- Wanasiasa wamemkashifu Rais kwa kukosa kuwaidhinisha baadhi ya majaji walioteuliwa na JSC
- Wengi wanashuku baadhi ya majaji waliachwa kwa kuwa walitoa uamuzi wa kuitipa nje BBI
- Seneta Murkomen amesema Rais ameweka mfano mbaya kwa marais watakaofuata kuwa wanaweza kuhitilafiana na uhuru wa mahakama
Hatua ya Rais Uhuru Kenyatta kukosa kuwateua baadhi ya majaji waliopendekezwa na tume ya huduma za mahakama JSC imewasha moto mitandaoni.
Wanasiasa wa mirengo tofauti waliweka tofauti zao kando na kukashifu hatua hiyo ya Rais wakisema ni ukiukaji mkubwa wa uhuru wa JSC.
Kupitia tangazo rasmi la serikali, Kenyatta aliwateua majaji 34 kati ya 41 ambao walikuwa wamependekezwa na JSC.
Hata hivyo, Ikulu ilikosa kuwaidhinisha majaji saba ambao ilidai wana doa na hivyo hawafai kuchukua nafasi hizo mpya.
Kati ya walioachwa nje ni majaji Joel Ngugi na George Odunga ambao walikuwa kwenye kikosi kilichoitema BBI nje kupitia kesi iliyokuwa Mahakama ya Juu.
Hatua ya Rais kuwaacha nje ilionekana kama kulipiza kisasi kutokana na uamuzi waliotoa.
Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo ambaye pia ni mwandani wa Raila Odinga alisema ni wakati Rais aambiwe wazi kuwa alifanya kosa.
"Kwa hili, Rais ni lazima aambiwe wazi kuwa hawezi kuidhinisha baadhi ya majaji baada ya pendekezo kutoka kwa JSC," alisema Otiende.
Mbunge wa Homa Bay Peter Kaluma naye alimkosoa Rais akisema ni kosa iwapo Rais alimtema Jaji Joel Ngugi kutokana na uamuzi aliofanya.
"'Sikubaliani na uamuzi kuhusu BBI lakini isiwe ndiyo sababu ya kukosa kuwateua Jaji Odunga na Ngugi wa Mahakama ya Juu," Kaluma alisema.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia [email protected] au WhatsaApp: 0732482690.
Tazama habari zaidi kutoka TUKO.co.ke