Mamlaka ya nchini Ghana inachunguza hali iliyosababisha kuzama kwa boti iliyouwa watoto nane wa shule kwenye Ziwa Volta katika eneo la kusini-mashariki.
Mamlaka za eneo hilo zilisema watoto wengine 12, waliokuwa ndani ya boti hiyo iliyopinduka siku ya Jumanne walinusurika.
Watoto hao walikuwa wakisafiri kutoka kijiji cha wavuvi cha Atikagome kwenda kwa jamii ya Wayokope ambako ndio shule yao ilipo.
Miili ya watoto wavulana watano na wasichana watatu wenye umri wa kati ya miaka mitano na 12 waliofariki imetolewa, Shirika la Kitaifa la Kukabiliana na Majanga la Ghana lilisema.
Tukio hilo limeibua wito kwa serikali kuboresha miundombinu ya usafiri katika maeneo ya vijijini.
Ajali za boti hutokea mara kwa mara kwenye Ziwa Volta kwa kiasi fulani kutokana na kujaa kupita kiasi, boti zilizojengwa vibaya, na kuwepo kwa vishina vya miti majini.
Mnamo Aprili mwaka jana, watu saba walifariki katika ajali kama hii.