Waathiriwa wa utapeli nchini Msumbiji wanasema wametapeliwa maelfu ya dola na mtu ambaye aliwaahidi kazi nchini Ureno.
Watu 13 katika mji mkuu wa Msumbiji, Maputo, kila mmoja alilipa kati ya dola za kimarekani 310 na 940, kwa mtu ambaye alisema atawapangia safari.
Mshukiwa raia wa Ureno aliyepatikana na paspoti 13 za Msumbiji anazomiliki amezuiliwa na polisi. Raia wengine wawili wa Msumbiji pia wanazuiliwa.
Mmoja wa waathiriwa alisema alikuwa na hamu ya kufanya kazi nchini Ureno, kama wengine alimlipa mshukiwa huyo pesa kupitia mtandao licha ya kutokutana naye ana kwa ana.
Mwanamke mwingine anasema kwa sasa hana kazi baada ya kusitisha kandarasi yake nchini Msumbiji kwa sababu alifikiri atakwenda Ureno.