WAZIRI wa Ulinzi na Masuala ya Maveterani, Tribert Mutabazi amesema miezi 10 imepita bila ya wanajeshi wa Burundi wanaolinda amani katika nchi za Somalia na Jamhuri ya Afrika ya Kati hawajalipwa posho zao.
Mutabazi alisema hayo wakati akieleza mafanikio ya robo mwaka ya wizara mjini Bujumbura mwishoni mwa wiki.
Hata hivyo, alisema kuchelewa huko kunatokana na ugonjwa wa covid-19 unaosababishwa na virusi vya corona vilivyovamia dunia.
Alisema fedha hizo zinazotolewa na Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika hazijawafakia walinzi wa amani wa nchi hiyo waliopo Somalia na Afrika ya Kati.
Waziri huyo alisema wanajeshi wa ujumbe wa kulinda amani Somalia (Amisom) wanatarajiwa kupata posho zao za miezi sita.
“Suala hilo liko mikononi mwa wafadhili na kama nchi hatuna tatizo kutuma fedha kwa wanajeshi hao, tunaahidi kuwa malipo mengine yatafanyika katika miezi ijayo,” alisema Mutabazi.