Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wakuu wa nchi za SADC kujadili ugaidi Msumbiji

16e333de23d0bc84adb10a6e234a69ef.jpeg Wakuu wa nchi za SADC kujadili ugaidi Msumbiji

Thu, 10 Jun 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

WAKUU wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wanatarajia kukutana mjini Maputo, Msumbiji kupokea taarifa ya vyombo vya ulinzi na usalama vya nchi hizo.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula, alisema mkutano utajadili namna ya kukabiliana na vikundi vya kigaidi katika Jimbo la Cabo Delgado, Kaskazini mwa Msumbiji.

Mulamula alibainisha hayo jana katika mkutano na waandishi wa habari mkoani Dar es Salaam.

Alisema SADC imeamua kubeba jukumu la kusimamia na kuhakikisha kuwa kwa pamoja, inapambana na hali ambayo si ya kivita, iliyosababishwa na vikundi vya kigaidi katika Jimbo la Cabo Delgado nchini humo.

Alisema vikundi hivyo vya kigaidi vimesababisha mauaji, uharibifu wa mali na kuwafanya wananchi wa Msumbiji kukimbia maeneo yao ili kujinusuru.

“Ninavyoongea kumekuwa na vikao si chini ya sita vya SADC tangu vurugu hizo zijitokeze. Wakuu wa nchi wamekuwa wakikutana Maputo nchini Msumbiji kila mwezi kujadili namna ya kusitisha vurugu za kigaidi huko Cabo Delgado,” alisema Mulamula.

Akaongeza: “Kumekuwa na maazimio kutokana na vikao hivyo, lakini kubwa zaidi ni kujipanga na ikibidi kupeleka kikosi cha pamoja cha SADC na kuitaka jumuiya ya kimataifa ijue kwamba, vita ya kupambana na vikundi vya kigaidi si ya nchi moja au mbili, bali ni jukumu la nchi zote za SADC na jumuiya ya kimataifa.”

Alitoa rai kwa nchi yoyote inayotaka kusaidia katika suala hilo ipitishe msaada wake SADC kwa ajili ya uratibu na kwamba, jumuiya hiyo ina chombo kilichoundwa kwa ajili ya kupambana na hali kama hiyo.

Mulamula alisema viongozi wa SADC hawajalala na kuna juhudi kubwa zinaendelea kuhakikisha amani inarejea nchini humo.

Chanzo: www.habarileo.co.tz