Siku tatu baada ya mlipuko kutokea eneo la Embakasi, wakaazi wameanza kutoroka eneo hilo tena kwa tuhuma za uvujaji wa gesi safi.
Ripoti za uvujaji wa gesi hiyo mpya zilianza kusambazwa Jumatatu, Februari 5, asubuhi na kuwalazimu watu kutafuta usalama katika maeneo jirani.
Serikali ya Kaunti ya Nairobi imewahakikishia wakaazi wa Embakasi kuwa eneo hilo ni salama kwani tayari wataalamu walikuwa wamedhibiti hali hiyo.
"Ni tahadhari tumechukua kwani tumeiita Mamlaka ya Kudhibiti Kawi na Petroli (EPRA) ili kubaini iwapo kuna tishio," Bramwel Simiyu, Afisa Mkuu wa Usimamizi wa Majanga wa Nairobi alinukuliwa akisema.
"Kuna ripoti kwamba kulikuwa na moto. Tumeweka huduma zetu katika hali ya dharura lakini hadi sasa hakuna sababu ya kutisha."
Bramwel Simiyu alihakikishia umma kuwa hakuna moto mpya uliotambuliwa na kwamba Serikali ya Kaunti itahakikisha kuwa kuna usalama kwa Wakenya.