Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wagombea Urais 61 wamewasilisha fomu zao Libya

Gadaffi Mtoto Wagombea Urais 61 wamewasilisha fomu zao Libya

Mon, 22 Nov 2021 Chanzo: BBC

Wagombea 61 wa urais wamewasilisha stakabadhi zao katika kinyang'anyiro cha kuiongoza Libya kabla ya tarehe ya mwisho ya Jumatatu, kulingana na tume ya uchaguzi.

Waziri Mkuu Abdelhamid Dabeiba alikuwa wa hivi punde zaidi kutangaza kuwania urais.

Fathi Bashagha, waziri wa zamani katika serikali ya umoja wa kitaifa ambaye anaungwa mkono sana magharibi mwa nchi hiyo, ni mshindani mwingine mwenye hadhi ya juu.

Spika wa sasa wa bunge Aguila Salah pia ni miongoni mwa watu wanaopendelewa zaidi.

Jenerali Khalifa Haftar, ambaye aliongoza kundi la waasi linalopinga serikali inayotambuliwa na Umoja wa Mataifa kabla ya kuafikia makubaliano ya amani mwaka jana, na Seif el Islam Gaddafi, mtoto wa kiongozi wa zamani wa Libya Muammar Ghaddafi, pia wanaonekana kuwa wagombea mashuhuri.

Waendesha mashtaka wa kijeshi nchini Libya wameitaka tume ya uchaguzi kusitisha kushughulikia maombi ya Jenerali Haftar na Bw Gaddafi hadi watakapohojiwa katika kesi za uhalifu zinazoletwa dhidi yao.

Jenerali Haftar anakabiliwa na mashtaka ya kisheria nchini Marekani kwa madai ya uhalifu wa kivita na Bw Gaddafi bado anasakwa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu tangu 2011 kwa madai ya uhalifu dhidi ya binadamu na mauaji.

Uchaguzi wa urais - ambao wengi wanatumai utarejesha utulivu na amani nchini humo tangu kuanguka kwa utawala wa Gaddafi miaka 10 iliyopita - utafanyika tarehe 24 Disemba.

Chanzo: BBC