- Wakazi walikuwa na wasiwasi kuwa wamefungiwa kutotoka au kuingia kaunti yao baada ya Rais kufunga gatuzi tano
- Ikulu ilisema sheria hiyo mpya ni ya kutotoka au kuingia kaunti hizo tano zikiwa pamoja
- Wakazi sasa watatembeleana lakini wasijaribu kuingia kaunti zingine 42
Serikali imefafanua kuwa wakazi wa kaunti tano zilizofungwa watakubaliwa kusafiri kutoka moja hadi nyingine mradi wasiende kwa hizo zingine 42.
Rais Uhuru Kenyatta Ijumaa Machi 26 alitangaza kufungwa kwa kaunti za Nakuru, Nairobi, KIambu, Machakos na Kajiado.
Wakenya waliingiwa na wasiwasi huku wakielewa ujumbe wa Rais kumaanisha kuwa hakuna kutoka kaunti moja hadi nyingine.
Hata hivyo, mkuu wa wafanyikazi katika Ikulu Nzioka Waita alisema wakazi wakaunti hizo tano wako huru kutembeleana.
"Tafadhali jueni amri ya kutotoka au kuingia ni ndani ya kaunti hizo tano za Nairobi, Nakuru, Kajiado, Machakos na Kiambu zikiwa pamoja. Kwa hivyo unaweza kutembea huru ndani ya kaunti hizo tano. Hata hivyo, hautaruhusiwa kuingia au kutoka kaunti hizo tano hadi zile nyingine," Waita alifafanua kwenye twitter.
Kutokana na hilo, Rais aliwekea kaunti hizo masharti makali kama vile masaa ya kafyu kuongezwa kutoka saa nne usiku na sasa itakuwa inaanza saa mbili.
Alipiga marufuku uuzaji wa pombe katika hoteli huku baa zote zikiagizwa kufungwa mara moja.
Hatua ya Rais iliwaweka wakazi wa maeneo hayo katika hali ya wasiwasi huku wakitaniwa mtandaoni.
Mchanganuzi wa kisiasa Mutahi Ngunyi alisema wakazi wako huru kucheza watakavyo na kuambukizana maradhi hayo hatari.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia [email protected] au WhatsaApp: 0732482690.
Tazama habari zaidi hapa TUKO.co.ke