Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amewataka waasi wa M23 katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kuheshimu makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyowekwa kuanza kutekelezwa siku ya Jumanne.
Antonio Guterres amekaribisha juhudi za kikanda na kimataifa zinazoongozwa na rais wa Angola na Umoja wa Afrika kujaribu kumaliza mzozo ambao tayari umewakimbiza mamia kwa maelfu.
Saa chache kabla ya usitishaji mapigano uliosimamiwa na Angola kuanza kutekelezwa, mapigano makali kati ya jeshi la Congo na kundi la M23 yameendelea katika jimbo la Kivu Kaskazini.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amelaani ghasia zote dhidi ya raia na kuhimiza makundi yote yenye silaha kuweka chini silaha zao bila masharti yoyote.
Bw Guterres amewataka wapiganaji wa M23 kuheshimu ahadi ya kusitisha mapigano ili kuwezesha kujiondoa kikamilifu na kwa ufanisi katika maeneo ambayo imeyamiliki, baadhi karibu na Goma, jiji kubwa zaidi mashariki mwa nchi.
Mzozo unaoendelea umesababisha mamia kwa maelfu kuyahama makazi yao katika mwaka uliopita na kusababisha shutuma kwamba Rwanda inafadhili waasi, jambo ambalo Kigali inakanusha