MAMLAKA ya Vifaa vya Tiba (KEMSA) imeanza awamu ya tatu ya usambazaji wa vyandarua vyenye dawa inayodumu kwa muda mrefu takribani milioni 10.1 ili kuongeza udhibiti wa ugonjwa wa malaria.
Awamu hiyo ya tatu ya ugawaji vyandarua lilianza Machi, mwaka jana kabla ya kusimama kutokana na mlipuko wa virusi vya corona na kisha kurejea tena Juni na Agosti.
Kaimu Ofisa Mkuu Mtendaji wa Kemsa, Edward Njoroge amesema awamu ya tatu ilianza mwishoni mwa mwezi uliopita na inatarajiwa kukamilika katikati ya mwezi huu.
Alisema awamu hiyo itaanza na walio katika mazingira magumu wakazi wa Lamu, Kwale, Mombasa, Kilifi na Tana River.
Alisema awamu ya kwanza Kemsa ilisambaza vyandarua zaidi ya milioni moja maeneo ya Kirinyaga, Baringo, Marsabit, Turkana na Vihiga na awamu ya pili walitoa 3,020,656 katika kaunti za Kisumu, Siaya, Homa Bay na Migori.
Awamu ya nne iliyopangwa kuanza Mei italenga Bomet, Nyamira, Kisii, Nandi, Kericho, Uasin Gichu, Taita Taveta, Pokot Magharibi na Trans Nzoia.