Vita vikali vya miezi tisa huko Sudan kati ya majenerali wawili hasimu vimepanuka zaidi hadi kwenye eneo la Urithi wa Dunia wa Shirika la UNESCO. Hii ni kwa mujibu wa ripoti ya shirika lisilo la kiserikali la The Regional Network for Cultural Rghts.
The Regional Network for Cultural Rghts limesema kuwa linalaani vikali mashambulizi ya Kikosi cha Msaada wa Haraka (RSF) cha wanamgambo wanaoongozwa na Jenerali Hamdan Dagalo katika maeneo ya kale ya Naqa na Musawwarat es- Sufra huko Sudan.
Kikosi cha Msaada wa Maraka (RSF) kinapigana vita dhidi ya wanajeshi watiifu kwa Mkuu wa Baraza la Uongozi wa Sudan, Jenerali Abdel Fattah al Burhan tangu mwezi Aprili mwaka jana.
Shirika hilo lisilo la kiserikali limesema kuwa wapiganaji wa RSF wameshambulia maeneo hayo ya jimbo la kaskazini la Mto Nile. Kundi hilo la haki za kitamaduni limesema, vyanzo vya kuaminika, picha na video zilizochapishwa kwenye mitandao ya kijamii zinaonyesha mapigano kati ya jeshi la Sudan na RSF na kuonyesha maeneo palipojiri uporaji, uharibifu na wizi wazi. Majenerali wanaogombea madaraka nchini Sudan
Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa limesema kuwa maeneo ya kiakiolojia ya Kisiwa cha Meroe, kilichoko takriban kilomita 220 kutoka Khartoum, mji mkuu wa Sudan yalikuwa kitovu cha Ufalme wa Kush, na yana mapiramidi, mahekalu na makao ya maelfu ya miaka iliyopita.