Mawaziri wa Ulinzi, Amani na Usalama kutoka nchi wanachama wa Umoja wa Afrika wameazimia kuanzisha jeshi la pamoja na kituo ili kupambana na changamoto ya ugaidi katika nchi wanachama wa jumuiya hiyo.
Kauli hiyo imetolewa nchini Ethiopia na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt.Stegomena Tax baada ya kumalizika kwa Mkutano wa mawaziri hao ambao hapo awali ulitanguliwa na mkutano wa wataalamu ukijumuisha Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama kutoka nchi wanachama wa umoja huo.
“Tuna tatizo la ugaidi kusini mwa nchi yetu lakini likiwa zaidi upande wa Msumbiji, lakini kama mnavyofahamu tatizo la ugaidi sio la nchi moja na nguvu ya nchi moja peke yake inakua vigumu kutokana na jinsi magaidi wanavyofanya kazi zao.
"Tumejadili na kwa kutambua umuhimu wake imepelekea kuwa na pendekezo la kuanzisha kituo na jeshi la pamoja ambapo nchi wanachama watachangia askari ili kupambana na changamoto ya ugaidi lakini na changamoto nyingine za ulinzi na usalama kwa kubadilishana taarifa, uzoefu, kutoa mafunzo ambayo hiyo itaongeza nguvu katika mapambano hayo.”alisema Dkt. Tax.
Akizungumza juu ya ushirikiano wa nchi za Afrika kukabiliana na changamoto za uhalifu unaovuka mipaka, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni amesema wameweka mikakati mbalimbali huku akiweka wazi jitihada za pamoja katika kupambana na ugaidi, usafirishaji haramu wa binadamu na dawa za kulevya.