Waziri mkuu wa Uingereza, Rishi Sunak ameendelea kushuhudia mgawanyiko kutoka kwa chama chake cha Conservative kuhusu mpango wa kuanzisha tena sheria mpya ya kuwatuma watafuta hifadhi nchini Rwanda.
Sunak ambaye ameufanya mpango wa kuwapeleka watafuta nchini Rwanda kipao mbele chake, anapata pingamizi kutoka kwa baadhi ya wabunge wa chama chake ambao wanadai, Sunak anafahamu fika kwamba mpango huo hautafulu.
Hata hivyo zaidi ya wabunge 30 wa mrengo wa kulia wanaunga mkono sheria ya Sunak, kutaka kufanya vigumu yeyote kufika mahakamani kupinga watafuta hifadhi hao kusafirishwa hadi nchini Rwanda. Waziri wa zamani wa uhamiaji ambaye alijiuzulu mwezi uliopita Robert Jenrick ,na amabye anaongoza uasi dhidi ya sheria mpya, amesema sheria hiyo haitazuia watu kufika mahakama kupinga mpango huo ambao mahakama ya juu tayari ilisema ni kinyume cha sheria.
Baadhi ya wabunge hata hivyo wanadai kwamba Sunak ameshikwa mateka na chama chake hasa baada ya madai kuibuka kwamba alipinga mpango huo wakati akihudumu katika wizara ya fedha.
Uingereza inalenga kuwatuma watafuta hifadhi nchini Rwanda, na kuweka sheria inayozuia wahamiaji kuingia nchini humo kiholela.