- Mbunge huyo wa Embakasi Mashariki alitania kuwa Rais Uhuru Kenyatta alimnongonezea kwamba Raila atateuliwa kuwania urais wakati wa uchaguzi mkuu ujao
-Alimsifu Uhuru kwa kutia bidii kutimiza ahadi zake kwa Wakenya
- Uhuru na Raila walikuwa Kisumu pamoja na viongozi wengine wa kitaifa kuadhimisha Sikukuu ya 58 ya Madaraka Dei
Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino amedai kuwa kiongozi wa ODM Raila Odinga ataidhinishwa na Rais Uhuru Kenyatta kuwania urais 2022.
Katika posti kwenye Twitter Jumatano, Juni 2, Babu alimumiminia Uhuru sifa kwa kutia bidii kutimiza ahadi zake kwa Wakenya
Pia alisifu uhusiano wa sasa kati ya rais na Raila, akidai kuwa atapendekezwa kuwania urais 2022.
"Asante sana Rais Uhuru Kenyatta kwa kutia bidii kuwatekelezea Wakenya. Ngoja muone vile Uhuru ananingonezea kuwa Baba atakuwa rais 2022," aliandika Babu huku akipakia video ya Raila na Uhuru wakihutubia wakazi wa Gem, kaunti ya Siaya.
Akizungumza huko Kisumu wakati wa sherehe ya 58 ya Siku ya Madaraka, Uhuru alisema kuwa maridhiano yao yalilenga sana amani ya nchi kufuatia mvutano ulioshuhudiwa katika Uchaguzi Mkuuwa 2017.
Alisema kuwa aliwalenga viongozi waliokuwa na agenda sawia na yake ya kuwaleta Wakenya pamoja na kueneza amani.
Wakati huohuo Babu Owino alimsherehekea Mama Ida Odinga kwa kumsaidia kukua kiroho.
Siku chache zilizopita mbunge huyo alitembelea familia ya Odinga nyumbani kwao Bondo wakijiandaa kwa sherehe za Madaraka Dei mjini Kisumu.
Wakati huo, Babu alitenga muda kuwa na Ida akitumia mitandao ya kijamii kumshukuru kwa kumsaidia kukua katika kimaadili ya Kikristu.