Mamlaka nchini Uganda zimeripotiwa kusitisha marufuku ya hivi majuzi ya uuzaji wa nyama katika mji mkuu, Kampala, huku kukiwa na mlipuko wa ugonjwa kimeta.
Maafisa wa afya wiki iliyopita walikuwa wameweka marufuku na kuamuru kufungwa kwa maeneo yote ya kuchinja ili kupunguza kuenea kwa mlipuko huo.
Lakini Waziri wa Masuala ya Jiji la Kampala Minsa Kabanda siku ya Jumapili aliliambia gazeti la Daily Monitor kwamba marufuku hiyo imesitishwa huku serikali ikiendelea kutathmini athari za ugonjwa huo katika mji mkuu.
Bi Kabanda hata hivyo aliwataka watu kuhakikisha kuwa wanyama wamepimwa kabla ya kuchinjwa.
Wafanyabiashara walikuwa wamepinga marufuku hiyo na kuishutumu serikali kwa kushindwa kudhibiti ugonjwa huo.
Ugonjwa wa kimeta umeripotiwa katika wilaya 40 kote nchini Uganda, kulingana na vyombo vya habari vya ndani.