RAIS Yoweri Museveni amesema kuanzia mwezi huu serikali itaanza kutoa chanjo ya virusi vya corona, ikiwa ni mkakati wa kutafuta dawa ya virusi hivyo.
Akizungumza na wananchi mwishoni mwa wiki iliyopita, Rais Museveni alisema wana sayansi wa ndani wamefanya utafiti wa kinga saba na sita zinaendelea na majaribio huku moja ya kuongeza kinga ikiwa tayari kwa matumizi.
“Dawa tatu za mwanzo ni za kupambana na virusi kwa kuviua na kupunguza uharibifu wa virusi mwilini,” alisema.
Kwa mujibu wa Rais Museveni, watu kadhaa wameponywa, hivyo kuanzia Desemba 15, wagonjwa chini ya uangalizi mkali wa matibabu watajaribiwa dawa hiyo.
Alisema wanasayansi wamemueleza kuwa ndani ya siku 40 wagonjwa wa kutosha watakuwa wametibiwa hivyo kuwashawishi watu wengine kutumia kwani inafanya kazi dhidi ya covid-19 na virusi vingine.
Alisema aina ya nne ni ya kuboresha koo na ambayo inafungua mapafu ya mgonjwa (njia za hewa) bila kuhitaji kutumia vifaa vya kusaidia kupumua.
Hatua hiyo imekuja huku kukiwa na ripoti kwamba Taasisi ya Utafiti wa Virusi ya Uganda (UVRI) imeshirikiana na Imperial College London kuanza majaribio ya kwanza ya chanjo ya covid-19 nchini kabla ya mwisho wa mwaka huu