Ubalozi wa Ethiopia katika mji mkuu wa Sudan Khartoum umeshambuliwa kwa silaha nzito Jumanne asubuhi, balozi wa Ethiopia huko amethibitisha.
Hakuna majeruhi walioripotiwa katika shambulio hilo lakini jengo la ubalozi huo liliharibiwa kiasi, balozi wa Ethiopia nchini Sudan Yibeltal Ayimiro Alemu ameiambia BBC.
Jeshi laRapid Support Forces (RSF), ambalo limekuwa likipigana tangu Aprili 15, limelaumu jeshi la serikali kwa shambulio hilo.
Jeshi la Sudan halijazungumza lolote kuhusu shambulio hilo.
Si mara ya kwanza kwa ubalozi wa Ethiopia mjini Khartoum kushambuliwa.
Mfanyakazi wa ubalozi wa Ethiopia nchini Sudan aliambia BBC kuwa ubalozi huo ulishambuliwa kwa mashambulizi ya anga wiki tatu zilizopita na kumjeruhi mlinzi. Pia ilivunja madirisha ya jengo la ubalozi huo.
Zaidi ya watu 5,000 wamefariki katika mzozo huo na wengine milioni tano kutoroka makazi yao, kulingana na UN.