Katika muda wa miezi miwili tangu Marekani na Umoja wa Mataifa kusimamisha msaada wa chakula kwa eneo la Tigray lililoathiriwa na vita nchini Ethiopia, takriban watu 728 wamefariki dunia, kulingana na mamlaka ya eneo hilo.
Wengi wa waliokufa walikuwa watoto, akina mama wajawazito, na watu waliokuwa na hali za kiafya, anasema Gebrehiwot Gebregziaher wa Tume ya Kudhibiti Hatari ya Majanga katika jimbo la Tigray.
Anasema kwamba ingawa USAid na Shirika la Mpango wa Chakula la Umoja wa Mataifa (WFP) walisimamisha rasmi msaada mwezi Aprili - baada ya kugundua shehena zilikuwa zikiibiwa na kuuzwa - kwa kweli watu wengi wa Tigray walikuwa hawana msaada kwa muda mrefu zaidi.
Watu wanahisi "wanakufa kwa njaa gizani ingawa inatangazwa kwa ulimwengu [kwamba] amani inastawi," alisema Dk Gebrehiwot, akimaanisha makubaliano ya amani yaliyofanywa mjini Pretoria Novemba mwaka jana kati ya serikali ya Ethiopia na waasi wa TPLF baada ya miaka miwili ya vita vya wenyewe kwa wenyewe.