Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Tanzania yaongoza EA gharama nafuu intaneti

2998e2c62414c3c791011c6bf6d0f05b.jpeg Tanzania yaongoza EA gharama nafuu intaneti

Wed, 5 May 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

Kwa mwaka wa pili mfululizo, Tanzania imetajwa kuwa ni nchi ya kwanza Afrika Mashariki yenye bei nafuu katika mtandao wa internet katika simu.

Takwimu zilizotolewa na Mtandao wa Utafiti wa Cable ya nchini Uingereza zinaonesha kuwa, Tanzania imeendelea kukamata nafasi ya kwanza kwa unafuu wa gharama za data.

Ripoti hiyo yenye takwimu za dunia zilizokusanywa kuanzia Desemba 08,2020 hadi Februari 25,2021 inaonesha kuwa, Tanzania ina bando rahisi inayogharimu Dola za Marekani 0.75 (sawa na Sh 1,742.81) kwa gigabyte (GB) moja ikifuatiwa na Rwanda (Dola 1.25), Uganda (Dola 1.56) na Burundi (Dola 2.10).

Kenya ilikuwa ya pili mwaka jana ambapo bando iligharimu Dola za Marekeni 1.04 kwa kila GB, lakini kwa mwaka huu gharama zimepanda na kufikia Dola 2.25.

Katika Ripoti hiyo ya takwimu za bei za simu duniani 2021, inaelezwa kuwa, kwa sasa nchi ya Somalia haitoi tena mtandao wa bei nafuu barani Afrika, ikishika nafasi ya tatu, wakati Sudan ikishika nafasi ya kwanza na Algeria inashika nafasi ya pili.

Inaeleza kuwa nchini Sudan, gharama ya mtandao wa simu ni Dola 0.27, ikiwa ni bei nafuu kuliko nchi zote barani Afrika na ya tano duniani.

Algeria ni ya pili kwa Dola 0.51 na Somalia ya tatu kwa Dola 0.60.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Tanzania inatoza data ya bei rahisi zaidi Afrika Mashariki kwa Dola 0.75 kwa kila gigabyte (GB) ya data.

Mchambuzi wa Mawasiliano ya Wateja huko Cable, Dan Howdle, alisema nchi nyingi zenye data za bei nafuu zina miundombinu bora na hutoa huduma kwa kutoa data nyingi, na kushusha bei kwa kila GB.

Nigeria na Afrika Kusini zinaelezwa kutoza kiwango kikubwa cha data kutokana na kuwepo kwa idadi kubwa ya watumiaji.

Nigeria ni Dola 0.88 na Afrika Kusini Dola 2.67.

Hata hivyo, utafiti ulifafanua kwamba nchi nyingi katikati ya orodha zina miundombinu mizuri na masoko ya ushindani ya simu.

Inaelezwa kuwa nchi ya Israeli kwa sasa inatoa intaneti ya bei nafuu zaidi ulimwenguni kwa Dola 0.05, ikitoka nafasi ya pili mwaka jana huku India ikishuka kutoka nafasi ya kwanza mwaka jana hadi nafasi ya 28 mwaka huu kwa Dola 0.68.

Chanzo: www.habarileo.co.tz