Moto mkubwa katika kambi ya polisi nchini Misri umejeruhi takriban watu 38, kwa mujibu wa huduma za dharura na vyombo vya habari vya ndani.
Wazima moto walifanikiwa kuzuia moto huo katika kituo cha Ismailia, na hospitali za eneo hilo zinasubiri majeruhi.
Video zilizochapishwa kwenye mitandao ya kijamii zinaonyesha jengo hilo likiwa limeteketea kwa moto.
Uchunguzi kuhusu chanzo cha moto huo umeamriwa, kwa mujibu wa shirika la habari la AFP. Vyanzo vya ulinzi wa raia vilisema kuwa moto huo ulisababisha sehemu za makao makuu ya Kurugenzi ya Usalama kuanguka.
Wizara ya afya ya Misri imetuma ambulensi 50 na ndege mbili za kijeshi kwenye jengo hilo, huku takriban watu 24 wakipatiwa matibabu ya kukosa hewa pamoja na wawili walioungua.
Kuna hofu kwamba idadi ya watu waliojeruhiwa inaweza kuwa kubwa zaidi huku mwandishi mmoja wa habari wa Misri akiripoti kuwa kutokana na ukubwa wa moto huo, kunaweza kuwa na vifo.
Mashahidi wawili waliozungumza na shirika la habari la Reuters walisema kwamba wazima moto walijitahidi kudhibiti moto huo, lakini vyombo vya habari vya ndani vinasema kwamba baada ya zaidi ya saa tatu walifanikiwa kuuzuia.