Rais wa Somalia, Hassan Sheikh Mohamud, amesaini sheria ya kufuta makubaliano kati ya Ethiopia na eneo lililojitenga la Somaliland, hii ikiashiria kutoridhishwa na matumizi ya bandari ya Berbera, uamuzi unaoibua hofu ya kutokea mgogoro baina ya pande hizo mbili.
Rais Mohamud amesema sheria hiyo inabatilisha rasmi mkataba aliouita haramu ambao unaoipa Ethiopia uhuru wa kutumia bahari yake kwa huduma za biashara na kambi ya kijeshi kupitia Somaliland, eneo ambalo halitambuliki kimataifa kuwa huru.
Kupitia mtandao wake wa X, kiongozi huyo wa Somalia amesema kupitishwa kwa sheria hiyo ni ishara ya kulinda uhuru wa Somalia kwa mujibu wa sheria za kimataifa.
Makubaliano hayo yameibua mvutano katika eneo la Pembe ya Afrika, huku Umoja wa Afrika, Marekani, Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu, zikitaka kuwepo kwa utulivu na uhuru wa Somalia kuheshimiwa.
Ethiopia ilifungiwa kutumia eneo hilo baada ya Eritrea kujitawala na sasa utawala wa Addis Ababa unafanya biashara zake kupitia Djibouti.