Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Shule zaonywa kutopandisha ada

90bc0b2e86072a112da7a1aa90dc7ca8 Shule zaonywa kutopandisha ada

Tue, 6 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

WAZIRI wa Elimu nchini Rwanda, Valentine Uwamariya, amezionya shule kutopandisha ada wakati zitakapofunguliwa baada ya kufungwa kutokana na mlipuko wa virusi vya corona vinavyosababisha ugonjwa wa covid-19.

Akizungumza na waandishi wa habari juzi, waziri huyo alisema uamuzi wa kufungua shule ulitangazwa hivi karibuni na serikali na wizara hiyo kueleza awamu ya kwanza vitafunguliwa vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu katikati ya mwezi huu.

Hata hivyo, imeelezwa kuwa, kufunguliwa kwa shule kutategemea jinsi zilivyoweka mikakati ya kuzuia maambukizi ya virusi vya corona bila ya kuongeza ada.

Uwamariya alisema hakuna shule itakayoruhusiwa kuongeza ada kwa sababu yoyote na kwamba wizara na wadau wengine watafanya kazi pamoja kuhakikisha hali hiyo haitokei.

“Tunafahamu kuwa baadhi ya shule zinataka kuongeza ada kwa kisingizio cha kupata fedha zitakazowawezesha kutekeleza taratibu zinazotakiwa kujikinga na virusi vya corona, jambo ambalo siyo sawa, shule zinatakiwa kujua kuwa wazazi pia wameathirika kifedha kutokana na ugonjwa huo,” alisema.

Hata hivyo, waziri huyo alisema hatua hiyo haizuii wazazi kusaidia shule, lakini siyo kwa kuongeza ada kwa lengo la kuhakikisha watoto wanakuwa salama wakati wakiendelea na masomo na kwamba mwanafunzi hatakiwi kulipa ada tena kwa muhula huo endapo ameshalipa kabla ya shule kufungwa.

Waziri wa Afya, Dk Daniel Ngamije, alieleza baadhi ya taratibu zinazotakiwa kufuatwa na shule kufuata wakati huu ni wanafunzi na walimu kuvaa barakoa, kuwa na vifaa vya kupima joto, maeneo ya kuosha mikono kwa sabuni na vitakasa mikono, pamoja na vyumba viwili kwa ajili ya wanafunzi wanaohisiwa kuwa na covid-19 kutengwa.

Chanzo: habarileo.co.tz