SERIKALI ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) imefungua tena shule za msingi, sekondari na vyuo, baada ya kufungwa kwa muda mrefu kutokana na homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya corona (Covid-19).
Shule hizo awali zilipangwa kufunguliwa Agosti 3 mwaka huu, lakini kutokana na sababu za kiufundi na kiutawala zilisogezwa mbele. Waziri wa Elimu wa DRC, Willy Bakonga alisema kuwa taasisi za elimu zilifungwa mwezi Machi mwaka huu ili kukabiliana na kuenea kwa virusi vya corona vinavyosababisha homa kali ya mapafu.
Baada ya kufunguliwa kwa taasisi hizo, Rais Felix Tshisekedi alitembelea baadhi yake na kuishukuru Wizara ya Elimu kwa juhudi zake za kuhakikisha kwamba masomo yanarejea tena nchini humo.
Taasisi ya Anadolu ilimnukuu Rais Tshisekedi baada ya kutembelea Shule ya Sekondari ya Athenee De La Gombe Eligo akisema.“ Tunawaomba muwe waangalifu.
Tumeondoa hali ya dharura, lakini virusi bado vipo. Ni kweli kwamba vijana wana nguvu, lakini wanaweza kuwa wasambazaji.
Epukeni kushikana mikono, naweni mikono, fanyeni kila muwezalo kuepuka maambukizi, mnaweza kuhatarisha na kuziambukiza familia zenu.”
Hadi juzi nchi hiyo iliripoti kuwa na wagonjwa 9,489 wa Covid-19 na vifo 224.