JESHI la Polisi nchini Somalia limethibitisha vifo vya raia wanane katika shambulio la bomu la kujitoa muhanga katika mji mkuu wa Somalia Mogadishu. Watu wengine 17 wamejeruhiwa, ikiwemo watoto 13 kutoka shule jirani iliyopo karibu na eneo la tukio.
Mlipuaji wa kujitoa muhanga aliyekuwa akiendesha gari lililoja vilipuzi alilenga msafara wa magari ya kampuni binafsi ya vikosi vya usalama vya Duguf vilivyopatiwa kandarasi kulinda Umoja wa mataifa UN. Polisi haijaeleza iwapo wafanyakazi wa Umoja wa mataifa wamejeruhiwa katika shambulio hilo.
Vyombo vya habari nchini humo vimesema kuwa mlipuko huo umetokea wakati wa msongamano wa magari karibu na makutano yanayofahamika kama Kilometre Four Junction. Kundi lenye uhusiano na al-Qaeda la wanamgambo wa al-Shabab limethibitisha kutekeleza shambulio hilo.
Vyanzo vya habari vinavyounga mkono al-Shabab media vimesema wanamgambo hao waliwalenga maofisa wa kijeshi wazungu. Mara kwa mara Al-Shabab wamekuwa wakiwalenga maafisa wa vikosi vya usalama na serikali mjini Mogadishu.