Waziri wa Mambo ya Nje wa serikalli ya mpito ya Niger amesema kuwa, Ufaransa inatishia amani na usalama wa dunia nzima.
Televisheni ya Al Jazeera imemnukuu Waziri wa Mambo ya Nje wa serikalli ya mpito ya Niger akisema katika taarifa yake kwamba bodi inayoongoza ya nchi hiyo itatuma barua kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kulalamikia rasmi jambo hilo.
Amesema: Tutatuma barua kwa Antonio Guterres kuhusu ukiukaji wa sheria za kimataifa unaofanywa na Ufaransa na Jumuiya ya Kiuchumi ya Nchi za Afrika Magharibi ECOWAS.
Waziri wa Mambo ya Nje wa serikalli ya mpito ya Niger ameongeza kuwa, vikwazo vya ECOWAS dhidi ya nchi yake ni kinyume cha sheria na ni uvunjaji wa wazi wa haki za binadamu.
Wananchi wa Niger wakifurahia kutimuliwa mkoloni Mfaransa nchini mwao
Akizungumzia hatua za kiuadui zinazoendelea kuchukuliwa na dola la kikoloni la Ulaya yaani Ufaransa, Waziri wa Mambo ya Nje wa Niger amesema, Ufaransa ni tishio kwa usalama wa kimataifa na inatafuta kisingizio cha kuivamia kijeshi Niger.
Vilevile televisheni ya Al Jazeera imenukuu duru moja ya kijeshi ya Niger ikitangaza jana Ijumaa kwamba vikosi vya jeshi la Burkina Faso vimeingia nchini humo kwa ajili ya kutoa mafunzo ya kuendesha operesheni za kupambana na ugaidi.
Hayo yameripotiwa katika hali ambayo wanajeshi waliofanya mapinduzi nchini Niger wameapa kupambana vilivyo na uingiliaji wowote wa kijeshi wa kigeni, huku Burkina Faso na Mali nazo zikiwa zimeahidi kuiunga mkono serikali ya mpito ya Niamey, mji mkuu wa Niger.