KITUO Tiba cha Rwanda (RBC) kimepanga kutengeneza vifaa vitakavyowezesha watu kujipima wenyewe virusi vya corona kwa haraka ili kusaidia kukabiliana na kuenea kwa virusi hivyo nchini.
Mkurugenzi Mkuu wa RBC, Dk Sabin Nsanzimana alisema katika mtandao wa twitter kuwa, kituo hicho kinatarajia kuanza kutumia vipimo hivyo hivi karibuni.
"Ninaamini kujipima wenyewe kwa wananchi kutafanya iwe rahisi zaidi, haraka na kwa bei nafuu," alisema.
Alisema vipimo vya kujipima mwenyewe vinaweza kutumika mahali popote kwa kutumia majimaji yanayotoka puani na ni vya haraka kuliko vinavyotumiwa na wafanyakazi wa afya.
Vipimo hivyo vimekuwa vikitumika katika nchi nyingine za Ulaya kama Uingereza, Austria, Ujerumani na Ureno na hatua hiyo imefikiwa baada ya serikali kutangaza mipango ya kupunguza gharama katika kupima ugonjwa huo.
Nsanzimana alisema lengo ni kupunguza gharama za vipimo vya RDTs kufikia faranga 5,000 au 6,000 kutoka faranga 10,000.