Rais Paul Kagame wa Rwanda amesema endapo nchi za Afrika zitaendelea kutegemea misaada ya chanjo kutoka mataifa makubwa itafika siku hakutakua na msaada huo na hali itakua mbaya hivyo ni wakati sasa nchi za Afrika kuanza kujitegemea na kuzalisha chanjo zake.
Kauli ya Rais Kagame inakuja siku chache baada ya kampuni ya uzalisha wa chanjo za Pfizer (BioNTech) kutoka nchini Ujerumani kutangaza kwamba iko mbioni kujenga kiwanda cha kuzalisha chanjo kwenye nchi za Rwanda na Senegal.
“Inachukua muda mrefu sana kwa nchi za Afrika kupata misaada ya chanjo za Covid-19, na chanjo zinapofika tayari watu wengi wanakua kwenye hali mbaya kiafya, ndio mana ni muhimu kwa nchi zetu kutafuta njia ya kuanza kuzalisha chanjo hapa hapa." Amesema Kagame wakati akiongea na televisheni ya Taifa Sept. 5, 2021.
“Afrika ilikua ikipokea misaada kwa haraka kila linapotokea jambo la dharula, lakini kwenye janga hili la Corona zile nchi ambazo zimekua msaada kwa Afrika nazo zimepata shida kubwa zaidi. Hapo sasa ndipo wazo la kuanza kuzalisha chanjo zetu wenyewe linapotakiwa kufanyiwa kazi kwa haraka, haitakua msaada kwa Rwanda pekee au chanjo za Corona pekee, tutazalisha chanjo za magonjwa mbalimbali kwaajili ya bara zima la Afrika" Amesema Kagame.
Taarifa ya Shirika la Afya Duniani (WHO) mwezi uliopita imesema kuwa misaada ya chanjo kuja kwenye nchi za Afrika imeongezeka kwa kiasi kikubwa japokua ni kweli kulikua na tatizo la upatikanaji wa chanjo hizo kwa baadhi ya nchi.