Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Rwanda, Burundi zakutana kufufua uhusiano mzuri

E208770271d83203dfef413e1abeae76 Rwanda, Burundi zakutana kufufua uhusiano mzuri

Tue, 27 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MKUTANO wa kwanza rasmi wa viongozi wa ngazi za juu wa serikali ya Rwanda na Burundi umefanyika kwa lengo la kukuza mahusiano yaliyoharibika kuanzia mwaka 2015.

Maofisa wa Rwanda na Burundi walifanya mazungumzo hayo juzi katika mpaka wa nchi hizo mbili wa Nemba katika wilaya ya Bugesera.

Katika mazungumzo hayo, Waziri wa Mambo ya Ndani na Ushirikiano wa Kimataifa wa Rwanda, Vincent Biruta alimkaribisha mwenzake wa Burundi Waziri wa Mambo ya Ndani na Maendeleo ya Ushirikiano, Balozi Albert Shingiro.

Biruta aliambatana na Mkurugenzi Mkuu wa Masuala ya Afrika katika wizara hiyo, Shakilla Umutoni, Balozi wa Rwanda nchini Burundi, Fidele Munyeshyaka na Katibu Mkuu wa Huduma za Usalama wa Taifa na Intelejensia (NISS) Meja Jenerali Nzabamwita.

Katika ujumbe huo pia walikuwepo mkuu mpya wa upelelezi wa nje wa Rwanda, Kamishana Msaidizi wa Polisi, Lynder Nkuranga na Meya wa Wilaya ya Bugesera, Richard Mutabazi.

Kwa upande wake, Shingiro aliambatana na msaidizi wake, Bernard Ntahiraja, Waziri wa Sheria, Sylvestre Nyandwi, Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Ferdinard Bashikaho, Balozi wa Burundi nchini Rwanda, Dorothee Ndayiziga na ofisa kutoka ofisi ya Rais, Alfred Innocent.

Mawaziri hao wawili wazungumza na waandishi wa habari kabla ya kufanya mkutano wao wa ndani na kueleza kuwa wapo tayari kufanya mazungumzo yatakayosaidia kuimarisha uhusiano baina ya nchi hizo mbili.

“Tuna furaha kuwapokea nchini hapa na wazo la majadiliano haya siyo kwa sababu ni majirani lakini pia sisi ni marafiki,” alisema Biruta na kueleza kuwa hiyo ni hatua kubwa katika kurejesha uhusiano wao uliotetereka.

Alisema wapo tayari kwa mazungumzo yenye tija na wazi katika kutafuta suluhisho la migogoro inayoendelea baina ya nchi hizo mbili.

Naye Shingiro alisema wapo tayari kwa mazungumzo kuhakikisha mahusiano mema yanarejea baina ya nchi hizo jirani.

“Tumekuja hapa kama serikali ya Burundi kwa sababu tunataka kuimarisha uhusiano wetu uliozorota mwaka 2015,” alisema kabla ya kuingia kwenye mkutano wa majadiliano wa ndani.

Mkutano huo unafuatia wa awali kati ya viongozi wa majeshi na wakuu wa usalama wa nchi hizo uliofanyika Agosti mwaka huu katika Jimbo la Mashariki kwa ajili ya kujadiliana masuala ya ulinzi na usalama.

Chanzo: habarileo.co.tz