Jumuiya ya IGAD, juma hili imechapisha ripoti mpya kuhusu hali ya hewa, ikionya kuhusu mvua kubwa zinazotarajiwa kunyesha kwenye nchi wanachama kuanzia mwezi ujao.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, msimu mrefu wa mvua unatarajiwa kuanzia mwezi Machi hadi Mei na kwamba nchi zitashuhudia mvua kupita kiwango cha kawaida, ambapo zitachangia asilimia 60 ya mvua za mwaka mzima.
Wataalamu wanatabiri kuwa kati ya asilimia 55 na 65 za mvua hizo, zitanufaisha mataifa ya Kenya, Somali, Ethiopia, Sudan, Uganda, Burundi, Rwanda na Tanzania, mvua kubwa zaidi zikitarajiwa katikati mwa nchi ya Kenya.
Ripoti hii ya wataalamu kutoka kitengo cha mabadiliko ya tabia nchi cha jumuiya hiyo, inatoa ubashiri wa mwenendo wa mvua zitakavyokuwa kwenye nchi za Ukanda, hali ambayo inatajwa huenda ikawa ahueni kwa wakulima wa ukanda.
Aidha ripoti imeonya kuhusu vipindi kadhaa vya kiwango cha juu cha joto.