Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron amelaani kitendo cha vikosi vya jeshi nchini Sudan kumuweka kizuizini Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Abdalla Hamdok na baadhi ya viongozi waandamizi wa Serikali.
Mapema leo Wizara ya Habari ya nchini Sudan, imethibitisha kukamatwa kwa waziri huyo na kupelekwa kusikojulikana huku ikiaminika jeshi hilo limedhamiria kufanya mapinduzi kutokana na Taifa hilo kukosa utawala bora na misingi ya demokrasia.
Mpaka sasa waandamaji 12 wasiounga mkono kitendo cha jeshi kuwashikilia viongozi hao wamejeruhiwa katika maandamano yaliyotangazwa na ofisi ya Waziri Mkuu leo.
Aidha, Afisa wa Jeshi, Abdel Fattah al-Burhan anayeongoza baraza tawala la kugawana madaraka amesema jeshi litaendelea na mpito wa kidemokrasia hadi kukabidhiwa kwa serikali iliyochaguliwa ya raia.