Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Rais wa Senegal aahirisha uchaguzi

Rais Wa Senegal Aahirisha Uchaguzi Rais wa Senegal aahirisha uchaguzi

Mon, 5 Feb 2024 Chanzo: Voa

Saa chache kabla ya kampeni ya uchaguzi kuanza rasmi nchini Senegal leo Jumapili, Rais wa nchi hiyo Macky Sall ametangaza kuwa uchaguzi wa rais uliopangwa kufanyika Februari 25 umeahirishwa kwa muda usiojulikana, na kuchochea hasira miongoni mwa viongozi wa upinzani na kujiuzulu kwa waziri.

Katika hotuba yake kwa taifa Jumamosi, Sall amesema ameahirisha uchaguzi ambao ungeamua nani atakuwa mrithi wake, kutokana na malumbano kati ya bunge la taifa na mahakama ya katiba juu ya kupinga baadhi ya wagombea.

Wabunge wanawachunguza majaji wawili wa mahakama ya katiba ambao uadilifu wao katika mchakato wa uchaguzi umekuwa na mashaka.

“Nitaanzisha majadiliano ya kitaifa kuweka pamoja mazingira kwa ajili ya uchaguzi ulio huru, wazi na shirikishi,” Sall ameongeza bila kutangaza tarehe mpya ya uchaguzi.

Saa chache kabla ya tangazo la Sall, Abdou Latif Coulibaly, katibu mkuu wa serikali ambaye alihudumu kama msemaji wa serikali, alitangaza kujiuzulu.

Ni mara ya kwanza uchaguzi wa rais kuahirishwa nchini Senegal na hali hiyo itaongeza mvutano wa kisiasa nchini humo.

Jumuia ya nchi za Afrika Magharibi (ECOWAS) imeelezea wasiwasi wake juu ya sababu za kuahirisha uchaguzi huo, na kwenye mtandao wake wa X siku ya Jumamosi ilitoa wito wa majadiliano na kuharakisha mchakato wa kupanga tarehe mpya ya uchaguzi.

Chanzo: Voa