Rais wa Ethiopia, Sahle-Work Zewde anatarajiwa kuwasili nchini kesho kwa ziara ya kikazi ya siku moja na atalakiwa na mwenyeji wake rais Dk John Magufuli katika Uwanja wa Ndege wa Chato mkoani Geita.
Akizungumza kutoka wilayani Chato, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof Palamagamba Kabudi amesema lengo la ziara hiyo ni kuimarisha uhusiano baina ya nchi hizi mbili na kubadilishana mawazo ya kikanda yenye maslahi mapana kwa pande zote mbili.
“Ratiba ishapangwa ikiwemo mazungumzo ya faragha baina ya viongozi hao wawili na kama mnavyojua nchi hizi zinashirikiana katika mengi kama masuala ya ulinzi,utalii na hata ukuzaji wa lugha ya Kiswahili” amesema Prof Kabudi.
Aidha, Prof Kabudi amesema kuwa nchi hiyo imepiga hatua kubwa sana kwenye uzalishaji wa bidhaa za ngozi hivyo kupitia ziara hiyo anaamini watanzania watapata fursa ya kwenda nchini humo kujifunza namna bora ya utengenezaji wa bidhaa hizo.