Ofisi ya rais wa Afrika Kusini imepuuzilia mbali ripoti za mitandao ya kijamii zinazodai kuwa Rais Cyril Ramaphosa ni mgonjwa na amelazwa katika hospitali ya kijeshi katika mji mkuu wa Pretoria.
Hii ni baada ya Bw Ramaphosa kukosa kuhudhuria mkutano ulioandaliwa na chama tawala cha African National Congress (ANC) siku ya Jumapili katika jimbo la Mpumalanga.
ANC ilitangaza kuwa Bw Ramaphosa ameondolewa kwenye mkutano huo kutokana na "dharura" isiyoelezeka.
Tangazo hilo lilizua minong'ono na uvumi kuhusu afya ya rais.
"Rais yuko sawa, hakuwahi kulazwa hospitalini, na hakukuwa na dharura," msemaji wa rais Vincent Magwenya alishiriki ujumbe kwenye mtandao wa X (zamani Twitter) siku ya Jumapili.
Bw Magwenya alisema rais aliamua kujituliza nyumbani siku nzima "kabla ya wiki yenye shughuli nyingi", akitaja uvumi huo kuwa "mbaya".