Rais wa Rwanda, Paul Kagame amesema hakuna yeyote duniani, anayeweza kuingilia mambo ya ndani ya nchi yake.
Kauli ya Rais huyo inakuja wakati ambapo kumekuwa na shinikizo kutoka Marekani wakitaka kumwachilia huru mkosoaji wa serikali yake Paul Rusesabagina ambaye amefungwa jela miaka 25 kwa makosa ya ugaidi.
Akizungumza pembezoni mwa mkutano wa viongozi wa Afrika na Marekani amesisitiza kuwa mambo ya ndani ya taifa lake yatatatuliwa na suluhisho kutoka ndani ya taifa hilo la Afrika Mashariki.
“Tumeweka wazi kabisa hakuna mtu yeyote, pale popote atakayekuja kutushurutisha kuhusu nini cha kufanya na maisha yetu,” amesema rais Kagame.