Raia wawili wa Afrika Kusini wameuawa katika mzozo unaoendelea kati ya Israel na Hamas.
Idara ya Uhusiano wa Kimataifa na Ushirikiano wa Afrika Kusini (Dirco) ilitoa habari hiyo Ijumaa, lakini haikufichua ni nani waliofariki.
"Idara ya Uhusiano wa Kimataifa na Ushirikiano inaweza kuthibitisha kwamba raia wawili wa Afrika Kusini wamefariki katika mzozo huu unaoendelea kati ya Palestina na Israel," alisema msemaji wa Dirco Clayson Monyela.
"Mchakato wa uthibitishaji kwa sasa unaendelea kwa sababu mmoja wa watu hao ameripotiwa kuwa na nambari ya kitambulisho cha Israeli, kwa hivyo tunahitaji kubaini kama ana uraia pacha."
Akizungumza kwa niaba ya serikali, Bw Monyela alitoa rambirambi kwa jamaa za watu hao.
Alisema: "Shughuli zetu huko Ramallah na Tel Aviv ni kuratibu juhudi na pia kutoa usaidizi wa kibalozi na huduma kwa familia za raia wetu."
Vita hivyo vilianza baada ya wanamgambo wa Hamas kufanya shambulio baya dhidi ya Israel mwishoni mwa juma.
Zaidi ya watu 2,700 nchini Israel na Gaza wameuawa tangu wakati huo.