Wanawake wawili raia wa Uganda hawajulikani walipo baada ya jengo walilokuwa wakiishi katika mji wa Diyarbakir nchini Uturuki kuangushwa na tetemeko kali la ardhi lililotokea Jumatatu asubuhi.
Akitoa taarifa kuhusu raia wao Balozi wa Uganda nchini Uturuki Nusura Tiperu amesema wanawake waliopotea walikuwa wakiishi jengo moja na raia wengine wawili wa Uganda ambao kwa bahati wao wamenusurika katika janga hilo.
Raia mwingine wa Uganda Karara Ashraf ameokolewa katika mji wa Malatya na hivi sasa amelazwa hospitali kwa matibabu.
Waganda wengine watatu wamekwama katika mji wa Gaziantep na wamejihifadhi ndani ya magari, huku mwingine mmoja akiwa amekimbilia mji wa jirani.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uganda Henry Okello Oryem amesema kuwa raia wao wengi huwa hawajiandikishi kwenye balozi, hata hivyo amekadiria kuwepo kwa waganda takribani 6,000 nchini Uturuki wengi wao wakiishi katika miji ya Istanbul,Konya,Ankara,Izmir na Antalya ambayo hadi sasa ipo salama.
Hadi sasa inakadiriwa kuwa watu zaidi ya 20,000 wamepoteza maisha katika matetemeko mawili yaliyotokea Uturuki na Syria.