Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Polisi wengine 200 wa Kenya waelekea Haiti

Polisi Wengine 200 Wa Kenya Waelekea Haiti.png Polisi wengine 200 wa Kenya waelekea Haiti

Thu, 18 Jul 2024 Chanzo: Bbc

Maafisa wengine 200 wa polisi wa Kenya wameondoka kuelekea Haiti chini ya ujumbe unaoungwa mkono na Umoja wa Mataifa kujaribu kumaliza ghasia za magenge katika taifa hilo lenye mgogoro la Caribbean, maafisa wakuu wa polisi walisema Jumanne.

Kutumwa huko kumekuja baada ya taifa hilo la Afrika Mashariki kutuma maafisa 400 katika mji mkuu wa Haiti ulioharibiwa na ghasia Port-au-Prince mwezi Juni, ikiwa ni sehemu ya ombi lenye utata la kutuma baadhi ya polisi 1,000 kusaidia kuleta utulivu nchini humo.

Ahadi hiyo, iliyotolewa na Rais William Ruto, ambaye anajaribu kutuliza maandamano ya kuipinga serikali nyumbani, imekumbwa na changamoto za kisheria nchini Kenya.

"Tuna maafisa wa polisi 200 ambao waliondoka jana usiku, wanapaswa kutua Haiti leo asubuhi," afisa mmoja mkuu wa polisi aliambia AFP siku ya Jumanne.

"Wanaungana na wenzao ambao tayari wako huko." Chanzo kingine cha juu cha polisi kiliithibitishia AFP kwamba maafisa hao waliondoka Jumatatu usiku, wakisafiri kwa ndege ya kukodi, na kuongeza: "Wengine zaidi wataondoka hivi karibuni hadi tupate 1,000 wote.''

Taifa hilo la Afrika Mashariki linaongoza kikosi kinachotarajiwa kuwa na jumla ya wanajeshi 2,500.

Nchi nyingine, hasa za Afrika na Karibiani, pia zinachangia misheni hiyo, ambayo imebarikiwa lakini haidhibitiwi na Umoja wa Mataifa.

Mnamo Julai 1, Huduma ya Kitaifa ya Polisi ya Kenya ilitoa taarifa kukanusha uvumi kwamba maafisa saba waliuawa nchini Haiti.

Vikosi vilivyotumwa vilikuwa "vimepokelewa kwa uchangamfu", na "vyote vilikuwa salama na tayari kutekeleza majukumu yao wazi na mahususi," ilisema.

Walikuwa "wakifanya kazi kwa karibu na mwenyeji wao, Polisi wa Kitaifa wa Haiti, na hadi sasa wamechukua ramani ya kimkakati ya maeneo ambayo yana uwezekano wa kufanyia kazi na kufanya doria kadhaa za pamoja ndani ya Port-au-Prince".

Chanzo: Bbc