Naibu Rais William Ruto ameelezea gharama ya siasa aliyolipia baada ya kumuunga mkono kinara wa chama cha ODM Raila Odinga.
Kwenye ziara yake katika eneo la Pwani Ruto amelalamikia usaliti aliopata baada ya kushtakiwa katika mahakama ya ICC akipigania uongozi wa Raila hadi akawa waziri mkuu. Ruto anasema sasa ni zamu ya Rais Uhuru na Raila kurudisha mkono kwa kumuidhinisha awe Rais kwenye kinyang'anyiro cha Urais 2022. Naibu Rais William Ruto amelalamikia ukosefu wa uaminifu, usaliti, na unafiki katika azma yake ya kuwania kiti cha Urais mwaka wa 2022. Ruto amesema kwamba kuna njama inayopangwa ya kuzima mipango yake ya kuwania urais.
Ruto alilalama kuhusu kulaghaiwa, akisema kwamba Rais Uhuru na Raila walimsifia kuwa mtu mwema wakati alipowaunga mkono kutwaa viti vya uongozi, ila hatimaye wakamwona kama tapeli baada ya kujitokeza kuwania urais kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.
"Nilipiga kampeni za kumuunga mkono Raila hadi akawa waziri mkuu; wakati huo alisema mimi ni mzuri. Nilimsaidia rafiki yangu Uhuru Kenyatta hadi akawa rais, ilisemekana kwamba mimi ni mtu mzuri…sasa wamenipachika majina mbalimbali wakisema, Ruto sio kiongozi mzuri, Ruto ni tapeli, Ruto ni mwizi," alisema.
Raila amekuwa akihoji utajiri wa kupindukia wa Ruto, huku akimtaka aelezee bayana anakotoa mamilioni ya fedha anazotoa kwenye hafla za kuchangisha pesa kote nchini.
"Hawa ni fisi waliovalia mavazi ya kondoo, wakidai wanataka kuchangia vikundi vya akina mama...watu watasema mtu huyu ni mkarimu na mcha Mungu kwa kuwa anasaidia kanisa, akina mama na vijana, ila wanachangiwa pesa zilizoporwa za mlipa ushuru," Raila alisema.
Haya yanajiri mwezi mmoja baada ya Ruto kuahidi kuangalia maslahi ya Rais Uhuru na Raila pindi atakapokuwa Rais na kuwahimiza wamuunge mkono.