By RAMADHAN ELIASKipa namba moja wa timu ya Taifa ya Burundi, Jonathan Nahimana amesema maingizo mapya ndani ya kikosi chao yanampa hofu wanapoelekea kuikablii Taifa Stars katika mchezo wa kirafiki utakaofanyika Jumapili kwenye uwanja wa Benjamini Mkapa jijini Dar es Salaam.
Kipa huyo ambaye anaeidakia klabu ya Namungo FC inayoshiriki Ligi Kuu Bara amesema wachezaji wengi wanaounda kikosi chao wanacheza ligi yao ya ndani nchini Burundi tofauti na Taifa Stars ambayo ina wachezaji wenye uzoefu na mechi za kimataifa.
"Kikosi chetu cha sasa kina wachezaji wengi wapya ambao wengi wao wanacheza ligi ya nyumbani Burundi hivyo hawana uzoefu wa kutosha kwenye mechi za kimataifa kwahiyo inabidi tuwe makini kutokana na wachezaji wengi wa Taifa Stars kujuana zaidi tukizubaa wanaweza kutufunga," amesema Nahimana.
Pia Nahimana amesema anaamini siku tano za kambi jijini Dar es Salaam zitawaongezea kitu na kuufanya mchezo baina ya Taifa Stars kuwa wa kuvutia na wenye ushindani mkubwa.
"Naamini kambi yetu ya siku tano tunaweza kutengeneza muunganiko mzuri na kupata kikosi bora ambacho kitaingia uwanjani kupambana na kuliwakilisha vyema taifa letu," amesema Nahimana.
Burundi ambayo imeweka kambi hapa nchini kwenye hotel ya Seascape iliyopo Kunduchi jijini Dar es Salaam. ina nyota 11, wanaocheza soka la kulipwa nje ya nchi hiyo wakiwemo Nahimana, Nzigamasabo Steve na Bigirimana Blaise wanaoichezea Namungo FC.